Sakata la ESCROW: Magufuli mkamate Seth wa IPTL - LEKULE

Breaking

25 Jan 2016

Sakata la ESCROW: Magufuli mkamate Seth wa IPTL


JUMUIA ya Wanazuoni Watetezi wa Rasilimali nchini (JUWARA), imewataka wabunge wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania linalotarajia kuanza rasmi vikao vyake vya kujadili hotuba ya Rais aliyoitoa wakati wa kulizindua bunge hilo hapo kesho,
kumuomba na kumkumbusha Rais DK. John Pombe Magufuli kutoa agizo la kukamatwa mara moja kwa mfanyabiashara Harbinder Sing Sethi ambaye ni mmiliki wa kampuni ya IPTL/PAP inayoendesha mtambo wa kufua umeme wa dharura uliopo tegeta Salasala kama sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya Bunge lililopita .

Wanazuoni hao wamesema kuna kila sababu ya wabunge wa bunge hili la 11 kusimama imara ili kutetea rasilimali za taifa letu zinazoonekana kutafunwa na wajanja wachache wanaotumia visingizio dhaifu vya sheria na uwekezaji kwa kumtaka Rais John Magufuli aharakishe utekelezwaji wa maazimio hayo ya Bunge hasa azimio namba moja lililoitaka serikali kumchukulia hatua kali na kumkamata mmiliki wa Kampuni ya IPTL, Herbinder Sing Seth kwa makosa ya kulisababishia taifa hasara ya zaidi ya bilioni 320 kutokana na wizi uliofanyika katika akaunti ya TEGETA ESCROW.

Pia, jumuia hiyo imesema ina imani kubwa na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo huku ikimtaka awe mwangalifu na asiwe mtetezi wa IPTL safari hii kwa kuwa maamuzi ya bunge yalikuwa sahihi dhidi ya kampuni hiyo, ambayo imeisababishia hasara kubwa serikali kutokana na vitendo vyake vilivyofanya.

Wakizungumza na JAMVI LA HABARI, Mwenyekiti na Katibu wa Jumuia hiyo, Omary Kisambu na Mahmud Salibaba kila mmoja,wameonyesha kusikitishwa na kitendo cha serikali kumkumbatia mfanyabiashara huyo, anayelalamikiwa na watanzania wengi kwa kulitia hasara taifa kutokana na vitendo vyake alivyovifanya kwenye sakata nzima la akaunti ya Tegeta Escrow.

"Tunashangaa mpaka sasa mapendekezo na maazimio muhimu ya Bunge kuhusu TEGETA ESCROW hayajatekelezwa na badala yake wameishia kuwatoa kafala kina William Ngeleja na Anna Tibaijuka, hii haitakiwi kuachwa ipite hivi hivi, lazima kama vijana wasomi tusimame kidete kupigania taifa letu na rasilimali zake" alisema Mwenyekiti huyo.

Naye, Katibu wa Elimu na Mawasiliano wa Jumuia hiyo, Mahmud Salibaba amelinukuu azimio namba moja na kushangaa kuona serikali imekubali kutekeleza azimio namba nane wakaliacha azimio namba moja ambalo linahitaji utekelezaji tu.

Mahmud aliongeza kuwa azimio namba moja linasema
"Bwana Harbinder Singh Seth na wengine,Bunge linaazimia kwamba, TAKUKURU, Jeshi la Polisi na Vyombo vingine husika vya Ulinzi na Usalama, vichukue hatua stahiki kwa mujibu wa sheria za nchi yetu, dhidi ya watu wote waliotajwa na Taarifa Maalumu ya Kamati, kuhusika na vitendo vyote vya kijinai kuhusiana na Miamala ya Akaunti ya Escrow, na watu wengine watakaogundulika kufuatia uchunguzi mbalimbali unaoendelea kuhusika katika vitendo vya jinai". Aliinukuu.

Katibu huyo, alisema "Hatuna wasiwasi na Prof. muhongo, Tunaamini ana mapenzi mema na utayari wa kulitumikia taifa katika sekta hii, lakini kwenye hili tunamtaka aweke mbele maslahi ya Taifa na kamwe asigeuke kuwa mtetezi wa IPTL wala Sethi".

Wanazuoni hao wameendelea kuonyesha matumaini yao kwa Bunge hili huku wakiamini kwamba kama ilivyo kawaida ya mabunge yaliyotangulia, panapotokea masuala ya kitaifa yenye maslahi mapana kwa nchi basi wabunge wav yama vyote huungana na kuweka tofauti zao pembeni na kulisimamia taifa liokoe rasilimali zake.

IPTL/PAP YAMZUIA ZITTO KABWE KUZUNGUMZIA.
Wakati hayo yakiendelea, kampuni hiyo inayolalamikiwa kuingizia hasara ya mabilioni serikali na kupelekea kuwajibishwa kwa watumishi kadhaa wa umma, imejitokeza na kuwataka wabunge waache kulizungumzia suala hilo kwa kuwa bado lipo mahakamani.

Katika taarifa iliyosambazwa kama tangazo iliyosainiwa na Katibu na Mshauri mkuu wa sheria wa Kampuni hiyo, Joseph Makandege, imemtaka Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto kutokuendelea kulizungumzia suala hilo na kwamba aache mpango wake wa kutaka kulifufua upya suala hilo hasa bungeni kwa kuwa tayari kampuni hiyo imeshamshitaki katika kesi ya madai iliyopo mahakama kuu na kwamba haitakuwa busara kwa mbunge huyo kulizungumzia suala hilo ambalo yeye binafsi ana maslahi nalo.

Kadhalika taarifa hiyo inasema kwamba tayari serikali imejibu kupitia hotuba ya Rais mstaafu Jakaya kikwete pindi alipokuwa madarakani kuwa haipo tayari kumkamata Sethi wala kutaifisha mitambo hiyo kwa kuwa itasababisha kuanzishwa kwa mahusiano mabovu na wawekezaji, hivyo Makandege amesisitiza kwamba ni vema mbunge huyo na mbunge mwingine yoyote aachane na mpango wa kuliibua suala hilo bungeni. 

‘’kwa uelewa wetu mdogo kuhusu maswala haya, kauli ya Rais huwa ndio kauli ya mwisho na ni sawa na hukumu, na tayari Rais (Rais Mstaafu Kikwete) alishasema kuwa suala hilo haliwezekani ‘’. Ilisisitiza taarifa hiyo ya Makandege.

‘’katika hali ya kiubinaadamu, si vema kwenda bungeni kushusha lawana na tuhuma kuwatuhumu watu na ama kampuni ambazo zenyewe haziwezi kuingia bungeni kujitetea’’. Ilisema sehemu ya taarifa hiyo.

‘’Hata mheshimiwa Zitto alifanya makosa kujihusisha na suala la IPTL/PAP wakati akijua kuwa ameshtakiwa mahakamani na kwamba moja kwa moja anakuwa na mgogoro wa kimaslahi, japo hajatamka mahala popote kuwa ana mgogoro wa kimaslahi na sakata husika’’. Iliongeza sehemu ya taarifa hiyo

ZITTO KABWE AWAJIBU .
Naye mbunge wa Kigoma mjini ACT – WAZALENDO ambaye wakati wa mjadala wa sakata hilo la ESCROW alikuwa mwenyekiti wa kamati ya Bunge inayosimamia hesabu za serikali, amejibu taarifa hiyo kwa kusema ni ya uongo inayoambatana na uoga wa kuwajibishwa na bunge baada ya kugundua maovu yao na kwamba IPTL /PAP hawana mamlaka ya kisheria kumzuia mbunge kujadili swala lolote ndani ya bunge akiwa anatimiza wajibu wake wa kikatiba.

‘’Sikuwa na soma ripoti yangu wala kuwasilisha maoni yangu, nilikuwa nawasilisha ripoti ya kamati ya kudumu ya bunge kwa hiyo si sahihi kulihusisha swala lile na mambo binafsi’’inasema taarifa ya Zitto Kabwe

‘’Mpaka wakati nawasilisha taarifa ya kamati bungeni, sikuwa nimewahi kupokea hicho wanachosema ni shitaka lao kwangu, kwa kuwa tumesoma ripoti mwezi November mwaka 2014 na nimeletewa shitaka lao mwezi mei mwaka 2015, kwa hiyo sikuwa na mgogoro wowote wa kimaslahi kama wanavyotaka kuuaminisha umma’’. Iliongeza taarifa ya mbunge huyo.

Zitto aliongeza zaidi kwa kusema kwamba mpaka sasa hajapokea taarifa ya kimahakama ikimzuia kutokujadili hoja inayohusiana na yeye kujadili jambo linahusiana na IPTL/PAP na badala yake amepokea taarifa ya kesi ya madai ya fedha na hivyo haki zake za kutumia katiba kujadili maswala ya kitaifa ndani ya bunge zipo pale pale na kwamba ataendelea kuwawakilisha watanzania kwa kusimamia rasilimali za taifa.

Sakata la IPTL na akaunti ya ESCROW lilibua hisia mbali mbali wakati wa mjadala wake uliodumu kwa zaidi ya miezi saba mwaka juzi na kuhitimishwa mapema January mwaka jana baada ya Waziri Muhongo kujiuzulu

Credit: Jamvi La Habari

No comments: