Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli
akimkaribisha Balozi wa Israel hapa nchini Mheshimiwa Yahel Vilan,
Ikulu jijini Dar leo.…Wakifanya mazungumzo, Ikulu jijini Dar.
Rais Magufuli akiagana na Balozi Yahel Vilan, Ikulu jijini Dar leo.
Rais Magufuli akiagana na Balozi Yahel Vilan, Ikulu jijini Dar leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amemhakikishia Waziri Mkuu wa Israel
kuwa Serikali ya awamu ya tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ipo
tayari kushirikiana na kuimarisha zaidi mahusiano kati ya Tanzania na
Israel katika nyanja mbalimbali ili kuleta manufaa kwa pande zote.
Rais Magufuli amesema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi
wa Israel hapa nchini mwenye makazi yake Mjini Nairobi – Kenya
Mheshimiwa Yahel Vilan, Ikulu Jijini Dar es salaam.
“Natambua mahusiano mazuri yaliyopo
kati ya Tanzania na Israel, mahusiano haya ni muhimu sana kwa ustawi wa
nchi zetu mbili, nataka mahusiano haya yaimarishwe zaidi ” Alisema Dkt. Magufuli.
Aidha, Rais Magufuli ameahidi kuwa Tanzania itahakikisha inaanzisha ubalozi wake nchini Israel haraka iwezekanavyo.
Kwa upande wake Balozi wa Israel hapa
nchini Mheshimiwa Yahel Vilan pamoja na kumpongeza Rais Magufuli kwa
kazi kubwa na nzuri iliyofanywa na uongozi wake katika kipindi kifupi
cha miezi miwili tangu aingie madarakani amemhakikishia kuwa Israel
itaendelea kushirikiana na Tanzania na ipo tayari kuimarisha zaidi
mahusiano.
Balozi Vilan ametaja baadhi ya maeneo
ya ushirikiano katika uchumi kuwa ni pamoja na Kilimo, Maji, Ufugaji wa
Nyuki na Sayansi na Teknolojia huku akibainisha kuwa Israel imewaalika
Jumuiya ya wafanyabiashara wa Tanzania kushiriki katika Kongamano la
biashara kati ya Tanzania na Israel litakalofanyika Mjini Tel Aviv
nchini Israel, mwezi Septemba mwaka huu.
Balozi Vilan pia ameahidi kufikisha
ujumbe wa Rais Magufuli kwa Waziri Mkuu wa Israel Mheshimiwa Benjamin
Netanyahu na pia ameahidi kuanzisha ofisi ya kutoa huduma ya visa hapa
nchini haraka iwezekanavyo.
Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU.
Dar es salaam.
19 Januari, 2016
No comments:
Post a Comment