MKATAJI
vichwa vya raia kutoka mataifa ya magharibi katika kundi la kigaidi la
Dola ya Kiislam (IS), Mohammed Emwazi, ametangazwa kuuawa.
Emwazi
anatambuliwa zaidi kwa jina la Jihadi John, ndiye aliyekuwa akitumiwa
zaidi kwenye video ambazo zilikuwa zikioneshwa na kundi hilo wakati wa
kutekeleza mauaji ya raia wa mataifa ya magharibi walilokuwa wakikamatwa
na kundi hilo.
Raia
huyo wa Uingereza alikuwa akitafutwa kwa udi na uvumba na wanajeshi wa
mataifa ya magharibi kutokana na kuhusika zaidi katika kutesa na kuua
raia wa mataifa hayo walikokamatwa na kundi hilo.
IS
wametangaza kifo cha Emwazi katika jarida lao la mtandaoni lijulikanalo
kwa jina la Dabiq. Taarifa ya IS inaeleza kuwa mwanamgambo huyo aliuawa
kwenye shambulio lililotekelezwa na ndege zisizokuwa na rubani Novemba
mwaka jana.
Hata
hivyo, Marekani baada ya kufanya shambulio lake dhidi ya Emwazi mwaka
jana mjini Raqqa, ilieleza kutokuwa na uhakika wa kumuua mwanamgambo
huyo.
Emwazi
alionekana mara kwa mara kwenye video za kikatili za kundi hilo,
miongoni mwayo ni ile iliyoonesha akiwakata shingo mateka kutoka mataifa
ya magharibi wakiwemo Muingereza David Haines ambaye alikuwa mfanyakazi
wa shirika la kutoa misaada na Alan Henning ambaye alikuwa dereva wa
teksi.
Lakini
IS kwenye tangazo lao walimtaja Emwazi kwa jina la Abu Muharib
al-Muhajir kutokana na kupenda kulitumia ndani ya kundi hilo wakati wa
uhai wake.
IS wanaeleza kuwa Emwazi alifariki dunia Novemba 12 kwenye gari lililoshambuliwa na ndege zisizo na rubani katika mji wa Raqqa.
Waliweka picha ya Emwazi akionekana kutabasamu. Alizaliwa Kuwait mwaka 1988 na kuhamia Uingereza mwaka 1994.
No comments:
Post a Comment