Kesi Ya Askofu Gwajima Kuendelea Kusikilizwa Februari 24 - LEKULE

Breaking

28 Jan 2016

Kesi Ya Askofu Gwajima Kuendelea Kusikilizwa Februari 24



Mahama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, imesema itaendelea kusikiliza ushahidi wa Jamhuri katika kesi inayomkabili  Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima.

Gwajima anakabiliwa na tuhuma za kutoa lugha ya matusi dhidi ya  Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, kwamba ni mtoto, hana akili na mpuuzi. Anadaiwa kutoa maneno hayo.

Kesi hiyo ilipangwa kusikilizwa ushahidi huo jana lakini iliahirishwa baada ya Wakili wa Serikali Mwandamizi, Shadrack Kimaro, anayeendesha kesi hiyo kuwa mgonjwa.

Kimaro alitoa madai hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi, Cyprian Mkeha, anayesikiliza kesi hiyo.

Wakili wa utetezi Peter Kibatala, alidai kuwa hana pingamizi na maombi ya Jamhuri.

Hakimu Mkeha alisema kesi hiyo itaendelea kusikilizwa Februari 24, mwaka huu na dhamana ya mshtakiwa inaendelea.

Katika kesi ya msingi, Askofu Gwajima anadaiwa kuwa kati ya Machi 16 na 25, mwaka jana, katika viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe jijini Dar es Salaam, alitoa lugha ya matusi kwamba “mimi Askofu Gwajima nasema Askofu Pengo ni mpuuzi mmoja yule, mjinga mmoja, amekula nini yule, sijui amekula nini yule mtoto hana akili yule”.

Alidai kuwa Askofu Gwajima alitoa maneno hayo ya kufadhaisha dhidi ya Kardinali Pengo na kwamba yanaweza kusababisha uvunjifu wa amani.

No comments: