Ikulu Yaagiza Mtumishi Atakayefanya Kosa Aadhibiwe Hapohapo Alipo Badala Ya Kuhamishiwa Sehemu Nyingine ya Kazi - LEKULE

Breaking

3 Jan 2016

Ikulu Yaagiza Mtumishi Atakayefanya Kosa Aadhibiwe Hapohapo Alipo Badala Ya Kuhamishiwa Sehemu Nyingine ya Kazi

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue.
 
MAKATIBU Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu walioteuliwa na kuapishwa juzi wamekutana katika ukumbi wa mikutano wa Ikulu jijini Dar es Salaam kwa ajili ya semina elekezi iliyoongozwa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue.

Akizungumza kabla ya kuanza kwa mada zilizoandaliwa katika semina hiyo  jana, Katibu Mkuu Kiongozi Sefue, alisema semina hiyo ni ya kikazi zaidi na kwamba lengo la serikali ni kuhakikisha viongozi hao waandamizi wanatekeleza wajibu wa kusimamia utendaji kazi wa serikali vizuri.

Balozi Sefue alisema kila Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu anapaswa kutambua kuwa nafasi yake ni ya maamuzi, hivyo serikali inatarajia kuona wanafanya maamuzi kwa usahihi na kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zinazomuongoza kila mmoja katika majukumu yake.

Alisema Serikali ya Awamu ya Tano inawatarajia viongozi hao kuwa wasimamizi wazuri wa fedha za umma na kwamba haitarajii kuwepo kwa hati za ukaguzi wa mahesabu zenye kasoro.

Balozi Sefue aliongeza kuwa Makatibu Wakuu hao na Naibu Makatibu Wakuu ni mamlaka ya nidhamu katika wizara zao, hivyo serikali haitarajii kuona wanakuwa na kigugumizi katika kuchukua hatua dhidi ya watumishi watakaokuwa na makosa.

Aliwakumbusha pia kwamba haikubaliki kwa mtumishi aliyefanya makosa katika sehemu moja ya kazi, kuhamishiwa katika sehemu nyingine badala ya kuchukuliwa hatua palepale alipo.
 


No comments: