Makubwa ya mtoa siri wa Raisi Magufuli wa Hospital ya Muhimbili. - LEKULE

Breaking

5 Jan 2016

Makubwa ya mtoa siri wa Raisi Magufuli wa Hospital ya Muhimbili.



HANDAKI
Chacha Makenge.

DAR ES SALAAM: Yule mgonjwa anayeaminika ndiye aliyetoa siri ya kuharibika kwa mashine za CT Scan na MRI Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa Rais Dk. John Magufuli na wiki iliyopita kudai amelazwa chini, Chacha Makenge, amesababisha mapya kuibuka.

Wakizungumza na gazeti hili mwishoni mwa wiki iliyopita, maofisa uhusiano wa Taasisi ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu (Moi), Frank Matua na Patrick Mvungi kwa nyakati tofauti, walisema kuwa, mgonjwa huyo hakuwa na tatizo lolote la kiafya na alisharuhusiwa kuondoka hospitalini hapo.

IMG_0294Chacha Makenge akiwa Hospitali.

“Alipimwa, tena alikuwa mgonjwa wa kwanza kupimwa kwenye CT Scan baada ya kutengenezwa na kugundulika uti wake wa mgongo uliumia miaka mitatu iliyopita. Alipoulizwa alikiri kuumia Stakishari… Kwanza haiwezekani mgonjwa wa uti wa mgongo kumlaza chini,” alisema Matua.
Akaongeza kuwa, baada ya kuonekana hana tatizo, aliruhusiwa kwenda nyumbani lakini anakataa akidai hana pa kwenda. Ndipo alipowaeleza maofisa hao kuwa ana familia ipo Mugumu, Serengeti mkoani Mara.

“Tulimtafutia tiketi ya basi na fedha za matumizi ili aende kwao lakini siku ya safari alikataa kwenda akisema anakwenda msibani. Pia akaelekeza kuwa fedha tulizomtengea kwa safari wapewe wagonjwa wengine ziwasaidie.

“Baada ya siku kadhaa, akarudi hapa Moi. Tulipomkumbusha kuwa amesharuhusiwa, alikataa kuondoka, hatukumshusha kitandani.

Wagonjwa wanaokataa kwenda makwao baada ya kuruhusiwa hapa hospitali wapo wengi na hatuwafukuzi, in humanitarian ground (kibinadamu), tunawapa huduma zote za chakula na malazi kwa gharama za serikali hadi utaratibu mwingine utakapofanyika,” alisema Matua.

Alifafanua kuwa, baada ya kuona Chacha anawasumbua kwa tabia zake mbalimbali, walimchunguza, wakagundua alishawahi kuwa na jalada katika wodi ya wagonjwa wenye matatizo ya akili Muhimbili, hivyo sasa wanafanya utaratibu mwingine wa kumsaidia.

Wiki iliyopita, gazeti hili lilikwenda Muhimbili, Taasisi ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu (Moi) na kumkuta Chacha akiwa amelala chini na akadai ameshushwa kitandani.

Kwa kuona kuwa uwepo wake pale unaweza kusababisha kumchafua Rais Magufuli aliyesimamia zoezi la kupatikana kwa vitanda, gazeti hili liliandika habari zake ili uongozi wa hospitali hiyo uchukue hatua bila kujua kwamba huko nyuma mgonjwa huyo aliwahi kufunguliwa jalada kwenye wodi ya wagonjwa wa akili.

Hata hivyo, maofisa uhusiano wa taasisi hiyo hawakupatikana wakati huo kuzungumzia tukio hilo lililowaacha midomo wazi watu walioingia wodini humo siku hiyo ya tukio.

No comments: