Bunge Lamkingia Kifua Rais Magufuli - LEKULE

Breaking

7 Jan 2016

Bunge Lamkingia Kifua Rais Magufuli


BUNGE limetoa idhini kwa mawaziri walioteuliwa na Rais John Magufuli ambao hawajala kiapo cha ubunge kushiriki shughuli za kibunge.

Limesema wateule wa Rais Magufuli  katika nafasi za uwaziri ambao kwanza waliteuliwa kuwa wabunge watakula kiapo cha ubunge wakati wa mkutano wa pili wa Bunge la 11, ili kutimiza matakwa ya kikatiba na kanuni za Bunge kabla ya kuanza rasmi kutekeleza majukumu yao ndani ya Bunge.

Msimamo huo wa Bunge umetolewa jana na Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashilillah kuhusu  uhalali wa mawaziri hao kushiriki shughuli za kibunge kabla ya kuapishwa.

Dk. Kashilillah alisema Katiba na Kanuni za Bunge hazimzuii Rais kuteua wabunge na kuwapa nafasi za uwaziri, wakati ambao Bunge halikutani na badala yake amepewa mamlaka ya kikatiba katika Ibara ya 55 ya kuteua mtu kuwa waziri na Ibara ya 56 inampa mamlaka ya kumwapisha.

Alisema kwa muktadha huo, Katiba na Kanuni za Bunge haziweki mipaka ya wakati wabunge kuchaguliwa au kuteuliwa.

“Rais hafungwi na masharti yaliyo kwenye ibara ya 68 ya Katiba kuhusu kuwaapisha wabunge kabla ya kuanza kushiriki shughuli za Bunge kwa  sababu tafasili ya shughuli za Bunge imewekwa wazi na Ibara ya 63 ambayo kimsingi inasema ni shughuli za Bunge ndani ya Bunge na kamati zake.

“Hivi sasa Kamati za Bunge bado hazijaundwa na Spika mpaka mkutano wa pili wa Bunge la 11 utakapoanza Januari 26, mwaka huu. Lakini hata kama itatokea kamati inafanya kazi zake kabla ya Bunge kukutana, kama kuna waziri ambaye hajaapishwa kuwa mbunge, rais ana mamlaka ya kumkaimisha waziri mwingine ambaye amekwishaapishwa kuwa mbunge kushikiri shughuli hizo.

“Leo nimeongea na waandishi wa habari wengi sana walionipigia simu wakiulizia hili kwa sababu naona limekuwa na mjadala mkubwa. Haya mambo ya kibunge ni vizuri kuyaelewa kwanza kwa sababu hata Kanuni za Bunge zimetoa nguvu kwa kamati kujipangia utaratibu wake wa kazi na kuwaruhusu watu ambao si wabunge au wabunge ambao si wa wajumbe wa kamati husika kushiriki katika vikao,” alisema Dk. Kashilillah.


Alisema kwa ruhusa hiyo iliyotolewa na Kanuni ya 117 (8), mawaziri walioteuliwa na Rais Magufuli wanaweza kushiriki kwenye shughuli za Kamati za Bunge pasipo kuhesabiwa kuwa ni wajumbe rasmi.

No comments: