Ahukumiwa Miaka 30 Kwa Jaribio La Kumbaka Mpenzi Wake - LEKULE

Breaking

19 Jan 2016

Ahukumiwa Miaka 30 Kwa Jaribio La Kumbaka Mpenzi Wake



MAHAKAMA ya wilaya ya Mpanda mkoani Katavi imemhukumu mkazi wa Mtaa wa Mpanda Hoteli, Manispaa ya Mpanda, Frank Jonas (27) kutumikia kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la kutaka kumbaka binti wa miaka 17 .

Hukumu hiyo ilitolewa Ijumaa iliyopita na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mpanda, Chiganga Ntengwa. 

Baada ya hukumu hiyo, baadhi ya watu walioshuhudia hukumu hiyo walihamasika na kudai hawakujua kama kosa la kutaka kubaka linaweza kumfunga mtu miaka 30 jela.

Hakimu Ntengwa alitoa hukumu hiyo baada ya mshtakiwa kukiri kutenda kosa lake hilo.

Awali, kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Ongela Malifimbo, alidai kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Januari 9, mwaka huu, saa 8:00 mchana katika eneo la shule ya Sekondari Mwangaza mjini Mpanda.

Ilidaiwa siku ya tukio mshtakiwa alimvizia msichana huyo wakati alipokuwa akipita katika eneo hilo kisha akamburuta kwenye nyasi ndefu kwa nia ya kumbaka.

Mwendesha Mashitaka huyo, alieleza mahakamani hapo kuwa baada ya kumburuza mpenzi wake huyo kwenye nyasi hizo ndefu, alimchojoa kwa nguvu nguo zake, kisha alimlalia juu ya kifua chake huku msichana huyo akipiga mayowe ya kuomba msaada.

Alieleza watu waliokuwa karibu na eneo hilo baada ya kuwa wamesikia mayowe hayo na walifika kwenye eneo hilo la tukio, ambapo walikuta Jonas akiwa amemlalia kifuani msichana huyo huku akihangaika kumchojoa nguo za ndani.

Ilidaiwa kuwa watu hao, walilazimika kumchomoa kwa nguvu juu ya kifua cha msichana huyo huku mtuhumiwa akiwa anawasihi wamuachie kwani anamfanyia hivyo kwa vile ni mpenzi wake ambaye alikuwa amekula fedha zake.

Hata hivyo, walimwondoa kwa nguvu kumpeleka kwenye kituo cha Polisi cha Mpanda huku akiwa hajatimiza lengo lake la kumbaka msichana huyo. Katika utetezi wake mshitakiwa aliiomba mahakama impunguzie adhabu kwa kuwa alifanya hivyo kwa vile msichana huyo alikuwa ni mpenzi wake na alikuwa amekula fedha zake.

Maombi hayo yalipingwa na mwanasheria wa Serikali kwa kile alichodai kuwa hata kama alikuwa ni mpenzi wake hakutakiwa kutaka kumbaka.

No comments: