Serikali Yahimiza Ujenzi Wa Viwanda Vidogo Vidogo Nchini - LEKULE

Breaking

24 Dec 2015

Serikali Yahimiza Ujenzi Wa Viwanda Vidogo Vidogo Nchini


Serikali imesema kuwa Tanzania haiwezi kubadirika ikiwa mawazo ya watu hayatabadirika katika ujenzi wa viwanda vidogo nchini kote na kuondoa mawazo ya kujenga viwanda vikubwa kama vya wafanyanyabiashara wakubwa, kwa kuwa vinahitaji mtaji mkubwa wakati ajira zake ni chache.

Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mheshimiwa Seleman Jaffo alitoa kauli hiyo tarehe 22 Decemba, 2015 wakati alipotembelea taasisi zilizo chini ya Wizara yake ambazo ni  LAPF  na Bodi ya Mikopo ya Serikali za Mitaa zilizopo mjini Dodoma.
 
Alisema baadhi ya Watanzania wamekuwa na mawazo kuwa viwanda vikubwa ndiyo vyenye ajira nyingi wakati viwanda hivyo kwa sehemu kubwa vinatumia mashine wakati viwanda vidogo ndiyo vyenye uwezo wa kutoa ajira kwa watu wa kada ya chini kwa wingi.

 Naibu Waziri alitolea mfano wa nchi za China na India kuwa wananchi wao wamewekeza katika viwanda hadi vipo viwanda vya familia na maisha yanasonga kwa ubora mkubwa kuliko maeneo mengine ya dunia.

“Watu wanaamini kazi kubwa ni kujenga viwanda, Mheshimiwa Rais anataka viwanda vijengwe kwa wingi na hata chumba cha nyumba kinatosha kuwa ni kiwanda kidogo cha kufanya kazi yoyote na mtu akapata ajira, kwa hiyo wakati tunasubiri uwekezaji mkubwa, naomba tuanze na hivyo viwanda vidogo,” alisema Jaffo.
 
Aliwaagiza mifuko ya hifadhi ya jamii kuanza kujikita katika ujenzi na upanuzi wa viwanda vidogo kuliko kung’ang’ania kuwekeza katika majengo makubwa ambayo alikiri kuwa yanasaidia kuifanya mifuko hiyo ionekane kuwa ni hai.

Kwa upande wake Kaimu Katibu wa Bodi ya Mikopo ya Serikali za Mitaa Bibi Apolonia Chagaka, alisema kuwa bodi yao imejidhatiti kwa kiasi kikubwa na katika maeneo mbalimbali wamewekeza baada ya kuona mtaji wao umekuwa.

 Alitaja baadhi ya maeneo ambayo wamewekeza ni Mbeya katika ukumbi wa Benjamini Mkapa, Mbinga, Musoma, Lushoto, Moshi, na maeneo mengi ambayo bado wanaendelea na mchakato wa ujenzi hivi sasa.
 
Naye Kaimu Mkurugenzi wa LAPF bwana John Kida alisema kuwa mfuko huo mbali na kazi kubwa wanazofanya ambazo zinahusiana na fedha, lakini bado wameendelea kukua na kuongeza mtaji kutoka 450 bilioni hadi kufikia 983 bilioni.


Kida alitaja changamoto inayokwamisha mifuko mingine ni kitendo cha serikali kutokulipa madeni makubwa baada ya mifuko kufanya kazi ikiwemo majengo ya utawala, miundombinu yote iliyofanywa katika Chuo cha Serikali za Mitaa Hombolo.

No comments: