Nyumba ya Jay Dee yapigwa mnada - LEKULE

Breaking

5 Jul 2015

Nyumba ya Jay Dee yapigwa mnada

Kampuni ya udalali ya MEM Auctioneers and General Brokers inapiga mnada wa nyumba ya mwanamuziki nyota wa bongo fleva, Lady Jay Dee, baada ya kushindwa kulipa deni alilokopa kutoka taasisi ya fedha ya EFC Tanzania Limited.
Kwa mujibu wa tangazo lililotolewa jana katika moja ya magazeti ya kila siku, mnada huo utafanyika saa 5:00 asubuhi kwenye eneo la kiwanja hicho lililopo Mivumoni.
“Kwa idhini tuliyopewa na EFC Tanzania Limited tutauza kwa mnada wa hadhara, dhamana/nyumba ya mdaiwa wa benki hiyo,” linasema tangazo hilo.
“Mnada utafanyika tarehe 4/07/2015. Jina la mdaiwa/mdhamini- Judith Wambura Habash, dhamana.nyumba itakayouzwa-Kiwanja Plot No. 54BLK4, Mivumoni Kinondoni Dar es salaam, tarehe ya mnada-4/07/2015 kuanzia saa 5:00 asubuhi na kuendelea,” linaongeza tangazo hilo.
Juhudi za kumpata mwimbaji huyo wa kibao cha “Machozi” hakuweza kupatikana jana kuzungumzia suala hilo, lakini Gadner Habash ambaye alikuwa na uhusiano na Jay Dee na ambaye jina lake limeandikwa kwenye tangazo hilo kama jina la tatu la mwanamuziki huyo, alisema hana taarifa hizo, hali kadhalika meneja wake.
Habari kutoka ndani ya taasisi hiyo zinasema kuwa mwanamuziki huyo alisitisha ghafla kulipa deni lake Juni mwaka jana bila taarifa yoyote na hata alipokuwa akitafutwa, hakuwa anapokea simu.
Kwa mujibu wa afisa kutoka kampuni ya MEM, nyumba hiyo iliyotumika kama dhamana ya mkopo, ipo kwenye kiwanja chenye ukubwa wa kilometa 901 za mraba, Tegeta Wazo na kina thamani ya Sh40 milioni.

No comments: