Mbunge Wa CHADEMA Ajivua Uanachama......Asema Kama CHADEMA Wanaubavu Wakalikomboe hilo Jimbo - LEKULE

Breaking

6 Jul 2015

Mbunge Wa CHADEMA Ajivua Uanachama......Asema Kama CHADEMA Wanaubavu Wakalikomboe hilo Jimbo

MBUNGE wa Mpanda Mjini, Said Arfi, jana aliwaaga wapiga kura wake akiwaeleza kuwa uanachama wake Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) utakoma mara baada ya kuvunjwa kwa Bunge la 10 mjini Dodoma.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Shule ya Msingi Kashato mjini hapa jana, Arfi, aliyekiwakilisha chama hicho kwa miaka 10 mfululizo, aliwaambia wananchi kuwa jimbo hilo litakuwa wazi wakati wowote wiki ijayo.
  
“Kama Chadema wana ubavu, waje walikomboe jimbo hili. Mimi ninaifahamu Chadema kuliko mtu yeyote mkoani Katavi kwani nilikuwa Makamu Mwenyekiti (Bara), na sasa nitamuunga mkono yeyote anayefaa kuwa mrithi wangu,” alisema Arfi na kushangiliwa.
  
Mkutano huo uliohudhuriwa na umati mkubwa, ulikuwa chini ya ulinzi mkali wa polisi kutokana na kuzagaa kwa taarifa za kutaka kufanyiwa fujo kwa Mbunge huyo na watu wanaoaminika kuwa wafuasi wa Chadema.
  
Arfi alisema hatogombea tena Mpanda Mjini; “Lakini nipo tayari kuvaa shati la kijani au la zambarau kumpigia debe mgombea yeyote katika jimbo hili. Ninawajua Chadema na kama wakiendelea kunifuatafuata, nitasema yote.”
  
Kauli hiyo ilitafsiriwa kuwa Arfi sasa atafanya kampeni akiwa CCM au ACT Wazalendo dhidi ya Chadema katika Jimbo la Mpanda Mjini, ambalo kabla yake halikuwahi kutawala na Mbunge mmoja kwa miaka 10 mfululizo.
  
Hii ni mara ya kwanza kwa Arfi kuweka hadharani mustakabali wake kisiasa, lakini kauli yake ya kuwa tayari kuvaa shati la kijana inakwenda tofauti na fununu zilizozagaa mjini hapa kuwa huenda akajiunga na ACT Wazalendo, chama kinachoongozwa na swahiba wake, Zitto Kabwe.
  
Ikumbukwe kuwa mara baada ya Chadema kutangaza kumvua nyadhifa zote Zitto takriban miaka miwili iliyopita, mara moja Arfi alitangaza kuajiuzulu nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa Chadema.

No comments: