Atiwa Mbaroni Akituhumiwa Kumuua Baba Yake kwa Shoka - LEKULE

Breaking

3 Jul 2015

Atiwa Mbaroni Akituhumiwa Kumuua Baba Yake kwa Shoka

MKAZI wa kijiji cha Igongwa wilayani Maswa mkoani Simiyu, Majingwa Ndushi (32) amekamatwa na jeshi la Polisi baada ya kutoroka akikwepa kufikishwa mahakamani kwa tuhuma ya kumuua baba yake mzazi, Ndushi Majingwa (65) kwa kumkata na shoka kichwani.
 
Mbele ya mahakama hiyo, ilidaiwa na Mwendesha Mashtaka wa jeshi hilo, Mkaguzi wa polisi Nassibu Swedy, kuwa mshtakiwa huyo alitenda kosa hilo, Mei 30 mwaka huu, saa tatu asubuhi kijijini hapo.
 
Alidai kuwa, kabla ya kufanya mauaji hayo mshtakiwa huyo alifika nyumbani kwa baba yake akiwa na shoka mkononi na kumkuta akiwa amekaa kwenye kiti na kisha kuanza kulumbana kwa maneno na hivyo kushindwa kuelewana, ndipo alipomshambulia kwa kumkata kwa shoka kichwani na kufa papo hapo.
 
Swedy alidai mahakamani hapo mbele ya Hakimu Tumain Marwa, kuwa chanzo cha mauaji hayo ni mgogoro wa muda mrefu wa kifamilia kati ya marehemu na mwanae huyo.
 
Alisema mara baada ya kufanya tukio hilo alitoroka lakini baada ya muda mfupi, alikamatwa na kisha kufikishwa katika kituo cha polisi cha wilaya ya Maswa.
 

Hata hivyo, mshitakiwa hakutakiwa kujibu lolote kwa sababu mahakama hiyo, haina uwezo wa kusikiliza kesi za mauaji na hivyo kesi hiyo itatajwa tena Julai 15, mwaka huu, na mshitakiwa amepelekwa rumande.

No comments: