Afande Sele aeleza atakavyokuwa tofauti na wasanii wengine walioingia bungeni - LEKULE

Breaking

2 Jul 2015

Afande Sele aeleza atakavyokuwa tofauti na wasanii wengine walioingia bungeni

Afande Sele amesema akiingia bungeni hawezi kuwasahau wasanii wenzake kama walivyosahauliwa na wasanii wabunge waliotangulia kuingia mjengoni.

Rapper huyo  atawania kiti cha ubunge wa jimbo la Morogoro Mjini kwa tiketi cha ya chama cha ACT na amesemakuwa akiingia bungeni wasanii watarajie mambo makubwa kutoka kwake.
 
“Lengo langu kubwa kwa wasanii ni kupigania haki za wasanii,” Amesema  Afande Sele
 
“Nimegundua tukizungumzia haki za wasanii kwenye muziki kwa kuimba tu, hakuna kitachofanyika. Viongozi hawana shinikizo la kutekeleza, wanazungumzia tu kidogo halafu wanaacha.
 
 "Lakini nimeona ukiingia bungeni wasanii tutashiriki moja kwa moja kwenye utungaji sheria za nchi.
 
 "Suala la haki za wasanii nitakuwa niko nalo karibu sana na nitalipigania kwa namna yoyote kwa sababu nipo kwenye chombo cha maamuzi na nina rungu mkononi,” ameongeza msanii huyo.
 
“Lakini leo hii hata nikiwa nazungumza sina silaha yoyote, lakini tukiingia bungeni tunaweza kupaza sauti na zikasikika kwa sababu tupo kwenye chombo cha sheria na kina mamlaka na uwezo. 
 
"Unajua kila anayeingia bungeni unakuta baadaye anabadilika, mimi nina upeo mkubwa tofauti na wabunge wanaomaliza muda wao. Inaonyesha waliingia kwenye siasa kwaajili ya kutafuta maslahi. Kwahiyo wasanii watarajie kuona sheria za haki miliki zikipatikana au zile zilizopo zikifanyiwa marekebisho,” amesisitiza.
 
“Kwa sasa hivi bungeni hakuna mtu mwenye uchungu na sanaa, wasanii ambao walibahatika kuwa wabunge wameingia bungeni nao wamegeuka mafisadi vilevile.
 
"Wamekuwa wawekezaji wa biashara, wamedharau shida za wasanii. KwaHiyo mimi nafikiri bungeni kulikuwa hakuna wasanii ambao wanatuwakilisha, wasanii tunaotaka kuingia bungeni sasa hivi tuna wito. Kwahiyo watu wategemee kuona mabadiliko makubwa sana kwenye sanaa.”
 
Katika hatua nyingine, Afande amesema kwa sasa hatoweza kutoa wimbo wowote mpaka uchaguzi utakapopita.
 

“Ningependa sana mashabiki wa muziki wangu wasubiri uchaguzi upite ndio wasikie kazi mpya kwa sababu tayari akili na mawazo na malengo yangu yapo kwenye uchaguzi. Mimi nimeona nisiwa-disturb kwa kitu chochote mpaka uchaguzi upite. 
 
"Kwa sababu hili ni jambo muhimu sana linatokea kwenye taifa na ni maisha yao. Kwahiyo watu wajitokeze kujiandikisha pamoja na kupiga kura ili kuwachagua viongozi wanaowataka.”

No comments: